Kwa Mujibu wa Ripoti ya Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) -ABNA- Jiji la Tanga, Tanzania – Uwanja wa Michezo wa Mkwakwani umefurika watu kutoka kila kona ya Mkoa wa Tanga na nje ya Tanga, ili kushiriki kwa kwa kuona kwa macho na kusikiliza kwa masikio yao Qur'an Tukufu ikisomwa kwa njia ya Tajweed katika Kongamano la Qur’an Tukufu lililofanyika leo hii katika Uwanja huo. Kongamano hili lilihudhuriwa na wasomaji bingwa wa Tajweed kutoka nchini Iran na ndani ya Tanzania, ambapo walitoa usomaji mzuri wa Qur’an Tukufu ulioleta msisimko mkubwa miongoni mwa hadhira.
Mgeni rasmi wa Kongamano hilo, Mheshimiwa Batilda Burian, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, alitoa pongezi zake kwa ajili ya tukio hili la kipekee linaloonyesha umuhimu wa Qur’an Tukufu katika jamii. Aidha, alishukuru taasisi zote zilizoshirikiana kuandaa Kongamano hili kwa mafanikio makubwa, na kupongeza ushirikiano wao wa dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Burian alisema kuwa Kongamano kama hili linaboresha uelewa wa Qur’an na kuhamasisha umoja na amani miongoni mwa wananchi wa Tanga na Tanzania kwa ujumla.
Hafla hii imetambulika kama mojawapo ya shughuli muhimu za kiroho na kitamaduni katika mkoa wa Tanga, ikionyesha mshikamano wa kikanda na kimataifa katika kuenzi na kusambaza mafundisho ya Qur’an Tukufu.
Tumekuwekea hapo chini picha zaidi za tukio hili adhimu
Your Comment